Pages

 

Friday, July 6, 2012

IJUE TEKNOLOJIA MPYA YA GOLINI KWA UFASAHA

0 comments

Hawk-Eye


Washabiki wa soka wanaofuatilia kwa makini Ligi Kuu ya Uingereza Premier League,wataanza kuiona teknolojia ya golini ikitumika kwenye ligi hiyo ifikapo mwezi Januari mwakani baada ya Bodi ya Kimataifa ya Vyama vya Soka Ulimwenguni (IFAB) kutia tiki matumizi ya teknolojia hiyo katikati ya wiki.

IFAB(International FA Board)imeingiza teknolojia hiyo kuwa moja ya sheria zitakazoendesha mchezo huo,na kufungua ukurasa mpya kabisa katika historia ya mchezo huo unaopendwa zaidi duniani

Mifumo miwili ya teknolojia hiyo ndio iliyopitishwa na kuruhusiwa kutumika baada ya majaribio mengi ya kisayansi kuwa yamefanyika.Mifumo hiyo Hawk-Eye na GoalRef inafanya kazi hivi:

HAWK-EYE.
Ni mfumo unaotegemea kamera,ambao ulitengenezwa na kampuni ya Uingereza ya Hawkeye,na kununuliwa na kampuni ya Kijapan ya Sony mwaka jana,teknolojia ambayo kwa muda imekuwa ikisaidia maamuzi kwenye michezo ya kriketi na tennis

Kamera 6 au 7 zenye uwezo wa kupiga picha kwa kasi ya ajabu zitafungwa pande zote mbili za uwanja na nyingine juu,zitakuwa na kazi ya kufuatilia mpira kila utakapokwenda ndani ya uwanja,kompyuta yenye uwezo wa kusoma taarifa kwa usahihi wa hali ya juu itakuwa ikipokea picha kutoka kwenye kamera hizo,kuzitafsiri kwa kasi na hapo hapo kutuma matokeo kwenye kifaa mfano wa saa ambacho mwamuzi atavaa mkononi kama kinavyoonekana pichani.
Kitu ambacho badomkinatia shaka ni iwapo kamera hizo zitafanya kazi kwa ufanisi iwapo mpira utakuwa umekumbatiwa na golikipa katika jitihada za kuwahi kuokoa.

Ingekuwa jambo zuri iwapo picha zinazotoka kwenye kamera hizo zingerushwa kwenye `replay`(picha za marudio) za kwenye TV pale unapotokea utata ili na sisi watazamaji tushuhudie jinsi teknojia hiyo inavyofanya kazi,lakini bahati mbaya FIFA wamesisitiza kuwa picha hizo hazitaoneshwa, si kwenye TV za uwanjani tu, hata majumbani!Kitu pekee kitakachofanyika ni mwamuzi wa mchezo kupewa ishara na kifaa alichovaa iwapo mpira utavuka mstari wa goli.


GoalRef

 GOALREF

Teknolojia hii ina mfumo uliobuniwa kwa ushirikiano wa wataalam wa Denmark na Ujerumani,na imeundwa kwa mfumo wa sumaku maalum ambayo inauwezo wa kugundua iwapo mpira utavuka mstari wa goli.

Kamba  maalum ndogo ndogo 3 zenye sumaku zinawekwa kwa ndani kwenye mpira eneo kati ya gozi na blada na mpira utnapo vuka mstari wa goli sumaku hii iliyo ndani ya mpira hutoa ishara kwenye vifaa maalum (sensor) vilivyowekwa ndani ya nguzo ya juu na zile mbili za goli.

Zile sensor zinapopata taarifa kutoka kwenye sumaku huwa kama zimetekenywa na kutoa aina ya mawimbi ya umeme ambayo bila kuchelewa hudakwa na kompyuta ambayo nayo hupeleka taarifa kwenye kifaa kama saa atakachovaa mwamuzi mkononi mwake..yote hayo niliyoyataja hufanyika chini ya sekunde moja!

Hii teknolojia ya GoalRef inatarajiwa kuwa na gharama kidogo katika kununua na kuifunga kuliko ile ya Hawk-Eye,lakini kampuni zinazotengeneza mipira bado zinajishauri iwapo ni sahihi kuweka sumaku ndani ya mipira yao,ila wataalam wa GoalRef  wanaendelea kutoa ushawishi wa kitaalam kuthibitisha kuwa hakuna tatizo.

…………………JE UNA MAONI GANI MSHABIKI WA SOKA?
Read more...
 
Said Nuhu © 2012 SAID NUHU BLOGS. BLOG IMETENGENEZWA NA BongoClan blog designer nipigie 0658184797