Pages

 

Saturday, July 13, 2013

BODABODA TISHIO LA NDOA ZA WATU.

0 comments
Madereva  wa  bodaboda licha ya biashara ya kusafirisha abiria, wamezua tabia nyingine ya kufanya ngono na  wateja wao wa kike, hasa wanafunzi na wake za watu.
Imebainika kuwa baadhi ya madereva wa pikipiki maarufu kama bodaboda wanatumia usafiri huo kuwarubuni na kuwashawishi wanafunzi wa kike wa shule za msingi na sekondari na kufanya nao ngono.
Uchunguzi uliofanywa na Mwananchi Jumapili jijini Dar es Salaam katika Wilaya za Temeke, Ilala na Kinondononi, umebaini kuwa wanafunzi wengi wamejiingiza katika vitendo vya ngono baada ya kunaswa na ulaghai wa madreva bodaboda wengi wakiwa vijana wadogo.
Madereva hao wamekuwa wakifanya ngono na wanafunzi, baada ya kuahidi kuwasafirisha bure kwenda na kurudi kutoka shuleni, hasa kwa maeneo ambayo hakuna usafiri wa daladala au eneo lililo mbali na kituo cha basi wakati wa kutoka au kwenda shuleni.
Gazeti hili limebaini kwamba, baadhi ya walimu pia wamejiingiza katika mchezo huo mchafu na kufanya ngono na vijana wadogo wanaoendesha bodaboda.
Madereva hao wanaoonekana katika vituo vya daladala, huwafuata wanafunzi hao wanaosumbuliwa na shida ya usafiri wakikataliwa kupanda daladala makondakta wa daladala hasa wakati wa asubuhi na jioni.
“Njoo asubuhi utaona wanafunzi wanavyohangaika kupata usafiri, mtu amefika kituoni toka saa kumi na mbili hadi saa mbili bado yupo hapa kila basi linalokuja anaambiwa wanafunzi wametosha. Katika mazingira haya kwanini asirubuniwe na mtu wa bodaboda?” alihoji mmoja wa wazazi alijitambulisha kwa jina la Mwambene na kuongeza:
 “Kuna baadhi ya madereva ninawafahamu wana uhusiano na wanafunzi wawili hadi watatu, tena hawachagui mwanafunzi wa shule ya msingi au sekondari, lazima wazazi wawafuatilie watoto wao vinginevyo wanafunzi hawatamaliza masomo.”
Baadhi ya madereva bodaboda walisimulia wanavyowashawishi na kuwanasa wanafunzi, wakikiri kulitumia tatizo la usafiri wa kwenda na kurudi kutoka shuleni kuwapata kirahisi wanafunzi.
Akionekana kuvifurahia vitendo hivyo, mmoja wa madereva wa bodaboda katika kituo cha daladala cha Temeke mwisho, (jina tunalo) alisema baadhi ya wanafunzi wanaona ufahari kupelekwa shuleni kwa pikipiki jambo linalowafanya wawe tayari kukubali kufanya ngono.
“Wapo wanafunzi wanaopenda kuonekana wanatoka katika familia bora, ...hao ndiyo rahisi sana kuwapata, ukimpeleka shuleni mara ya kwanza, mara ya pili basi umemaliza mchezo,” alisema dereva huyo akijinasibu.
Alisema baadhi ya wanafunzi hutoka nyumbani kwao wakiaga wanakwenda shuleni lakini badala yake hukutana na madereva wa bodaboda ambao huwapeleka mafichoni na kufanya nao ngono.

Dereva mwingine wa bodaboda, mkazi wa Keko Machungwa, Elikunda Kileo alikiri kuwepo kwa matukio hayo akisimulia kuwa mmoja wa madereva wa bodaboda alipigwa na wananchi baada ya kukutwa akimtomasa mwanafunzi wa shule ya sekondari akiwa ndani ya mabanda ya kutengenezea samani.
Kwa mujibu wa Kileo, dereva huyo alimhaidi mwanafunzi kuwa angempeleka shuleni, lakini muda mfupi baadaye alimwingiza kwenye banda la mafundi seremala na kuanza kumdhalilisha kwa kumtomasa maeneo mbalimbali ya mwili wake.
“Jamaa aliingia na mwanafunzi kwenye banda la mafundi seremala linalomilikiwa na kaka yake, cha kushangaza tuliona anataka kufanya vitu vya ajabu, maana alianza kumshikashika yule binti, ingawa binti mwenyewe hakuwa na wasiwasi wowote,” alisema Kileo na kuongeza kuwa:
“Mafundi wakamwambia aondoke, lakini jamaa akaanza kuwatukana ndipo walipoamua kumpa kipigo.”
Dereva mwingine wa bodaboda anayefanya kazi Mbezi Msumi alikiri kuwa na uhusiano na wanafunzi wawili na mwalimu mmoja kutokana na kuwapa lifti ya pikipiki mara kwa mara.
“Si unajua tena kaka, mi ninao wawili, mmoja kidato cha pili mwingine cha nne, tena nina mwalimu, wote nawachukua, ingawa wakati mwingine naona aibu kuwa naye kwani yeye ni mkubwa kuliko mimi,” alisema dereva huyo.
Hata hiyo, baadhi ya madereva wa bodaboda waliwatupia lawama wanafunzi kuwa wao ndiyo wanaowashawishi madereva hao kufanya nao ngono.
Renatus Kitwana dereva wa bodaboda anaefanya biashara yake katika kituo cha Ukonga Mombasa, alisema baadhi ya wanafunzi hufika kituoni hapo na kusimama muda mrefu wakiwasubiri ‘watu wao’. “Kuna wanafunzi huja hapa kutafuta pikipiki, lakini wakiwakosa watu wanaowataka watasubiri muda mrefu hadi jamaa watakaporudi kitu kinachoonyesha kuwa nao wanapenda kufanya vitendo hivyo,” alisema Kitwana.
Wanafunzi wananena
Agnes Tarimo, mwanafunzi aliyehitimu kidato cha nne mwaka 2012 katika shule ya sekondari Jangwani, alisema kuwa kuna baadhi ya wanafunzi wasichana walikuwa wanakwenda shuleni wakiwa na nguo za kubadilisha kwenye mabegi yao kwa ajili ya kutoka shuleni na kuingia mitaani bila kujulikana.
“Kuna wanafunzi wenzetu walikuwa wanabeba nguo za kubadilisha kwenye mabegi yao. Jamaa wa bodaboda wakija wanakwenda nao sehemu wanabadilisha nguo, halafu wanakwenda kufanya mambo yao huko mafichoni,” alisema Agnes.
Naye Mwanaidi Seif mwanafunzi wa kidato cha Tatu, shule ya sekondari Perfect Vision, alisema kuwa  tamaa ya usafiri wa bure (lifti) na chips imewafanya wanafunzi wengi kujihusisha na vitendo vya ngono
 
“Wanafunzi wengi wanatamaa ya kupata vitu vizuri, wengi wamejikuta wakifanya ngono na kupata mimba kwa kupenda kupewa lifti na chipsi,” alisema Mwanaidi.
Kaimu Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Mtakatifu Anthony, Mbagala ambaye hakutaka jina lake liandikwe gazetini kwa kuwa si msemaji wa shule, alisema kuwa suala la wanafunzi kuwa na uhusiano na madereva siyo geni na kwamba lipo tangu siku nyingi.
“Ingawa hapa shuleni hatujapata kesi kama hiyo, lakini suala hilo si geni lipo toka siku nyingi na siyo madereva wa bodaboda tu wanaofanya vitendo hivyo hata madereva wa taxi na daladala,” alisema mwalimu huyo. Alisema baadhi ya madereva wanaojihusisha na ‘mchezo’ huo ni watu wazima ambao umri wao ni sawa na wazazi wa wanafunzi wanafanya nao ngono.
“Wengine ni watu wazima kabisa sawa na baba zao... wazazi lazima wawaangalie sana watoto wao hali ni mbaya,” alisema mwalimu huyo.
Wazazi walonga
Meshack Kilave, mkazi wa Tabata ambaye binti yake anasomoma kidato cha kwanza kati shule ya sekondari Magomeni alisema tatizo la wanafunzi kujihusisha kimapenzi na madereva lipo toka siku nyingi na kwamba wanafunzi wanabuni mbinu mpya kila siku za kuwaficha wazazi wao.
“Baadhi ya wanafunzi huaga nyumbani kuwa wanakwenda kwenye masomo ya ziada kumbe wameshatekwa na jamaa wa bodaboda,” alisema Kilave.
Alishauri wazazi kuwafuatilia kwa kuwauliza watoto wanapowabaini kumiliki vitu ambavyo hawakukinunua wazazi.
“Wazazi watawafuatilie watoto wao kwa karibu, watabaini mambo mengi yaliyofichika, badala ya kukaa na kusikia ukiambiwa mwanao ni mjamzito.”
Naye Stumai Ng’ingo, mkazi wa Kongowe alisema ameshtushwa na taarifa za madereva wa bodaboda kufanya ngono na wanafunzi akieleza kuwa ndio kwanza amezisikia taarifa hizo.
“Ndiyo ninasikia kwa mara ya kwanza kuwa madereva wanaweza kufanya hivyo, sijui kama wadogo zangu wanaosoma sekondari wanaweza kupona wasitumbukie mikononi mwa hao jamaa,” alisema Stumai. George Daffa, mkazi wa Mtoni kwa Azizi Ali aliwatupia lawama baadhi ya wazazi kuwa wanachangia watoto wao kufanya vitendo vibaya kutokana na kukosa uangalizi wa kutosha.
“ Baadhi ya wazazi wanahitaji kubadilika, waache tabia ya kudhani wakishawalipia watoto  wao ada basi jukumu la kuwafuatilia limeisha,” alisema Daffa

0 comments:

Post a Comment

 
Said Nuhu © 2012 SAID NUHU BLOGS. BLOG IMETENGENEZWA NA BongoClan blog designer nipigie 0658184797